MRADI
WA KUSWAHILISHA PROGRAMU HURIA
WARSHA
YA ARUSHA 1-5 NOVEMBA 2004-11-22
KATEGORIA ZA KISARUFI KATIKA UUNDAJI WA MANENO.
(GRAMMATICAL
CATEGORIES IN TERM CREATION)
G.
Mrikaria
Katika lugha
yoyote kuna aina mbalimbali za maneno. Maneno haya yamepewa kategoria kulingana
na matumizi yao au uhusiano baina ya aina moja ya maneno na aina nyingine za
maneno.
Shughuli ya uundaji wa msamiati mpya imekuwa ikifanyika wakati wote
binadamu alipokuwa akitumia lugha kufikisha ujumbe wake. Wakati wote amekuwa
akitunga maneno mapya kueleza mambo au dhana mpya alizobuni au kuziona. Maneno
haya yamekuwa yakiwakilisha vitu au vitendo alivyofanya au kusikia. Maneno
yamekuwa yakiundwa mara yalipohitajika kwa kuwa hayakuwepo katika lugha.
Kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, dhana mbalimbali zimekuwa
zikibuniwa na vitu vingi vimekuwa vikiundwa ambavyo havikuwepo katika utamaduni
wa lugha husika, hivyo imelazimu vitafutiwe na kupewa maneno au majina ya
kuviwakilisha.
Katika Kiswahili
uundaji wa maneno hufanyika kwa njia mbalimbali. Njia ya kwanza ni ile ya
kukopa maneno kutoka katika lugha
nyingine. Njia hii mara nyingi hufanyika kwa kutohoa maneno ya lugha nyingine
na kuyapatia mazingira ya utamkaji katika Kiswahili, kwa mfano, televisheni
limekopwa toka katika Kiingereza television, kompyuta limekopwa toka katika
neno computer. Mifano hiyo michache inaonyesha jinsi njia hii ya uundaji wa
maneno ilivyotumika katika Kiswahili.
Njia nyingine ni
ile kuunda maneno mapya kwa kutumia njia ya uambishaji au unyambulishaji wa
maneno yaliyo katika Kiswahili. Mfano neno cheza
ukiliwekea kiambishi ku- unapata neno
kucheza na ukiweka kiambishi m- mwanzoni na kubadili kiambishi cha
mwisho a na kiambishi o utapata neno mchezo. Njia hii imekuwa ikitumika sana katika Kiswahili ikitumika
kama njia ya kuzalisha maneno kwa kutumia maneno yanayotumika katika lugha
yenyewe bila kwenda nje ya lugha.
Njia nyingine ni
ile ya kufupisha maneno marefu na kuunga silabi za mwanzo ili kupata neno moja
mfano, chakula cha jioni kuwa cha- + jio = chajio. Pia inawezekana kuunganisha
maneno mawili au zaidi ili kupata neno moja mfano pakashume, mbwa-mwitu nk.
Vilevile maneno
yanaweza kuundwa kwa kubadili kategoria za maneno. Kwa njia hii tutaona jinsi
kategoria za maneno mbalimbali zinavyotumika kuzalisha maneno ya kategoria
nyingine.
Katika utaratibu
wa kuunda maneno mapya, moja ya njia itumikayo kuzalisha maneno mapya ni ile ya
kuchukua neno lililo katika kategoria moja na kuunda neno au maneno ya
kategoria kama hiyo au maneno ya kategoria nyingine. Njia hii imekuwa ikitumika
sana katika uundaji wa maneno ya Kiswahili. Maneno yanaweza kuundwa kwa
kuangalia sifa maalumu za vitu au matukio fulani yaliyotokea. Kutokana na
kitendo kinachofanywa na kitu nacho kitu hicho huweza kupewa jina kulingana na
kitendo hicho. Mfano kitendo anachofanya mdudu anayetoboa punje za mahindi au
maharage, watu wameamua kusema kuwa anabungua,
hivyo naye mdudu huyo akapewa jina la bungua.
Neno baki ni kitenzi cha kinachoeleza hali ya
mtu au kitu kutoondoka na pia ni nomino yenye maana ya salio.
chapa kama kitenzi humaanisha piga, na likitumiwa kama nomino
humaanisha alama maalumu inayowekwa kwenye kitu au bidhaa.
Baadhi ya maneno
yameonekana kuwa na uwezo wa kuzalisha maneno mengine na yale maneno
yaliyozalishwa nayo yameweza kuzalisha maneno ya aina nyingine. Kwa hali hiyo
tumeyaita yale maneno yaliyozalishwa moja kwa moja kutoka maneno ya msingi kuwa
yamezalishwa katika hatua ya kwanza. Yale maneno yaliyozalishwa kutokana na
maneno yaliyozalishwa katika hatua ya kwanza tumeyaita maneno yaliyozalishwa
katika hatua ya pili. Iwapo yatapatikana maneno yatakayozalishwa kutokana na
maneno yaliyozalishwa katika hatua ya pili tutayaita maneno yaliyozalishwa
katika hatua ya tatu.
Vitenzi ni aina ya
maneno yenye uwezo mkubwa kuliko maneno mengine kushiriki katika utaratibu wa
kuunda maneno mengine. Kitenzi kimoja kinaweza kutumika kuunda maneno ya
kategoria mbalimbali kama vile nomino, vielezi, vivumishi nk.
1. Kitenzi sikia kinaweza kuzalisha maneno kadhaa
katika hatua mbalimbali. Kinaweza kuzalisha maneno katika hatua ya kwanza, ya
pili na kuendelea kama ifuatavyo:
hatua ya kwanza
kinaweza kuzalisha maneno kama vile: msikiaji,
sikio, usikivu, sikiliza.
msikiaji (nm) - mtu anayesikia
sikio (nm) kiungo cha mwili kinachofanya kazi ya kusikia
usikivu (kl) hali au tabia ya kusikia
sikiliza (kt) pokea na dhibiti mawimbi ya
sauti kwa umakinifu.
Katika hatua ya
pili maneno yaliyozalishwa kutokana na neno la msingi nayo yanaweza kuzalisha
maneno mengine, kwa mfano maneno yafuatayo yanaweza kuzalisha maneno kama
ifuatavyo:
sikiliza linaweza
kuzaa maneno kama vile: msikilizaji na
usikilizaji, masikilizano.
msikilizaji (nm) mtu anayesikiliza
usikilizaji (nm) kitendo cha kusikiliza
masikilizano (nm) maelewano.
2. kitenzi tembea kwa hatua ya kwanza kinaweza
kuzalisha maneno kama vile: mtembeaji,
tembelea, tembeza, n.k.
mtembezi mtu mwenye tabia ya kutembea ovyo
utembeaji jinsi au namna ya kutembea
utembezi tabia ya kutembea ovyo
matembezi kitendo cha kutembea rasmi.
tembelea enda mahali kwa makusudi ya kumwona mtu au jambo
fulani
Katika hatua ya
pili maneno yafuatayo yanaweza kuzalisha maneno mengine kama ifuatavyo:
tembelea tembeleana, tembeleka, tembeleo,
utembeleaji, matembeleano
tembeza - mtembezi, utembezi, matembezi, utembezaji,
mtembezaji, tembezwa, tembezana.
3. kitenzi cheza kwa hatua ya kwanza kinaweza
kuunda maneno yafuatayo: mchezo,
uchezaji, mchezaji, mcheza, chezesha, chezwa.
mchezo jambo au tendo lifanywalo kwa ajili kuleta furaha au
hufanywa na zaidi ya mtu mmoja kwa ajili ya mashindano
uchezaji - kitendo cha kucheza
chezesha simamia mchezo
mcheza mtu anayecheza
mchezaji mtu anayecheza mchezo
katika hatua ya
pili maneno yafuatayo yanaweza kuzalishwa kutokana na neno lililozalishwa
katika hatua ya kwanza kama ifuatavyo:
chezesha mchezeshaji, uchezeshaji
4 tafuta kwa hatua ya mwanzo linaweza
kuzalisha maneno kama vile: utafutaji,
mtafutaji
utafutaji kitendo cha kutafuta
mtafutaji mtu anayetafuta
5 kokota mkokota,
mkokoto, mkokotoo, mkokotoaji, mkokotaji
6 cheka kwa hatua ya kwanza linaweza
kuzalisha maneno kama vile chekesha,
kicheko, cheko, chekea, chekwa, ucheshi, mcheshi, n.k.
Katika ya pili
neno lililozalishwa katika hatua ya kwanza linaweza kuzalisha maneno mengine
mfano, chekesha mchekeshaji,
uchekeshaji, kichekesho, chekeshea, chekeshwa
Utaona kuwa
vitenzi vinavyozalishwa kutokana na vitenzi vingine vinakuwa na uwezo zaidi wa
kuzalisha maneno mengine kuliko kategoria nyingine ya maneno.
2.2
Kutumia Nomino kuunda maneno mengine
Nomino pia huweza kuzalisha maneno ya kategoria sawa nazo na pia maneno ya
kategoria nyingine, kwa mfano:
taifa taifisha,
utaifishaji, taifishwa, taifisho
buku bukua
taabu taabisha, utaabishaji, taabika
sakafu sakafu, sakafia, sakafisha, usakafishaji,
msakafishaji
Vivumishi ni
kategoria nyingine ya maneno inayoweza kuzalisha maneno ya aina nyingine,
mfano:
refu refusha, urefu, marefu, refuka, kwa
hatua ya kwanza na kwa hatua ya pili: refusha inaweza kuzalisha maneno: urefushaji, marefusho, refushia, mrefushaji
nene nenepa
Kwa hatua ya pili
nenepa inaweza kuzalisha unenepaji,
nenepesha
Kwa hatua ya tatu
nenepesha inaweza kuzalisha unenepeshaji,
unenepeshwaji, mnenepeshaji
safi safisha, usafi, safisho kwa hatua ya
kwanza
Kwa hatua ya pili
usafi inaweza kuzalisha usafishaji,
msafishaji
zuri mzuri, uzuri
pole mpole, upole
bora ubora, boresha, uboreshaji, maboresho,
boreka
Vielezi ni kategoria
ya maneno ambayo huweza kuunda maneno ya aina nyingine. Kutokana na kielezi
tunaweza kuunda maneno mbalimbali na ya kategoria tofauti, Mfano:
haraka harakisha. Hapa kitenzi harakisha kimeundwa kutokana
na kielezi haraka.
Kwa hatua ya pili
harakisha inaweza kuzalisha neno uharakishaji,
harakisho
tayari tayarisha, utayari kwa hatua ya
kwanza ya uzalishaji
Kwa hatua ya pili
ya uzalishaji tayarisha inazaa utayarishaji,
mtayarishaji, matayarisho
karibu - kwa hatua
ya kwanza inazalisha ukaribu, karibia,
karibisha na kwa hatua ya pili neno karibisha linaweza kuzalisha makaribisho, ukaribishaji, makaribishano,
karibishana, karibishia
binafsi linaweza
kuzalisha ubinafsi, binafsisha,
ubinafsishaji
Mara nyingine
hutokea dhana au kitu kipya ikashindikana kupatiwa neno moja fupi
litakalofikisha ujumbe au kuwakilisha dhana husika. Kwa kawaida njia inatumiwa
katika kuunda maneno yenye kuleta utata kama huu kwa kuunganisha maneno mawili
au zaidi yenye kuhusika ili kuleta maana. Uunganishaji wa maneno kama haya
unaweza kufanyika kwa kuunganisha nomino na nomino, nomino na kivumishi au
kitenzi na nomino, n.k.
mwana + sheria -
mwanasheria
paka + shume - pakashume
kiazi + kitamu
kiazikitamu
kidole + tumbo -
kidoletumbo
mwana + mwali -
mwanamwali
mwana + nchi
mwananchi mwenyeji wa nchi fulani
viwavi + jeshi
viwavijeshi
hifadhi + data
hifadhidata
eneo + data
eneodata
kanzi + data -
kanzidata
Nomino huweza
kuunganishwa na kivumishi ili kuunda neno moja. Mifano ifuatayo inaweza
kudhihirisha usemi huu.
mwana + mkiwa
mwanamkiwa - yatima
mwana + haramu
mwanaharamu mtoto aliyezaliwa nje ya ndoa
jua + kali -
juakali
Miji + kenda
Mijikenda
mkwaju + nyuma
mkwajunyuma
mkwaju + mbele -
mkwajumbele
2.4.4 kitenzi + nomino
Kitenzi kinaweza
kuunganishwa pamoja na nomino ili kuunda neno jipya. Katika Kiswahili kuna
maneno kadha yaliyoundwa kwa njia hii, mfano:
chemsha + bongo
chemshabongo -
mpiga + mbizi
mpigambizi mzamaji chini ya maji
Njia ya
urudufishaji wa maneno hutumika pia sana kwa kurudia neno moja mara mbili. Mifano ni maneno kama vile:
piga linaweza kuzalisha neno
- pigapiga
kata linaweza kuzalisha neno
- katakata
choma - chomachoma
ponda - pondaponda
Njia mojawapo
inayotumika katika uundaji wa maneno ni kufupisha kikundi cha maneno ili kupata
neno moja. Njia hii hutumika zaidi katika kuonyesha kifupi cha majina ya
mashirika, magonjwa au hata dhana fulani, mfano:
Upungufu wa Kinga
Mwilini UKIMWI
Taasisi ya
Uchunguzi wa Kiswahili TUKI
Chama cha
Mapinduzi CCM
Chakula cha jioni
chajio
Taasisi ya
Kiswahili na Lugha za Kigeni TAKILUKI
Tawala za Mikoa na
Serikali za Mitaa TAMISEMI
Chama cha Netiboli
Tanzania CHANETA
Hivyo kwa kutumia njia utaona kuwa dhana inayowakilishwa
na mlolongo mrefu wa maneno inakuwa rahisi kutajwa kwa kutumia neno moja
lililofupishwa.
MAREJEO