MRADI WA
KUSWAHILISHA PROGRAMU HURIA
WARSHA YA ARUSHA
1-5 NOVEMBA 2004-11-22
MADA YA MAFUNZO
UUNDAJI WA
ISTILAHI: UZOEVU WA BARAZA LA KISWAHILI LA TAIFA (BAKITA)
na
P.C.K. Mtesigwa
UUNDAJI WA ISTILAHI: UZOEVU WA BARAZA LA KISWAHILI LA TAIFA (BAKITA)
1.0 Utangulizi
Jukumu kuu ambalo Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) limepewa kisheria kwa mujibu wa Sheria ya Bunge Na. 27 ya mwaka 1967 iliyoliunda ni kukuza, kuimarisha na kuendeleza Kiswahili hasa ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Katika marekebisho ya sheria hiyo yaliyofanyika mwaka 1983 kwa Sheria ya Bunge Na. 7, BAKITA limepewa uwezo wa kufuatilia na kusaidia ukuzaji wa Kiswahili katika nchi za nje pia. Kwa hiyo kazi zinapokuwa zimethibitishwa na BAKITA huzihusu pia juhudi za uendelezaji wa Kiswahili katika nchi za nje.
Kimsingi ukuzaji au uimarishaji wa lugha maana yake, kwa upande mmoja, ni utumiaji wa lugha hiyo kwa usahihi. Kwa mtazamo huo maana yake ni kuhakikisha kwamba kanuni za sarufi yake zinafuatwa. Lakini pamoja na hilo, kwa upande mwingine kuna suala la kuiwezesha lugha hiyo kukidhi mahitaji ya watumiaji wake wa kila hali na kila uwanja wa matumizi. Kusema kweli mojawapo ya vigezo vinavyotumika kujua kiwango cha kukomaa kwa lugha ni kupima jinsi inavyojimudu katika msamiati wake kukidhi matumizi katika nyanja mbalimbali zikiwemo nyanja maalumu za kitaalamu. Ili kutimiza lengo hilo hapan budi msamiati wake ukuzwe na kusambaa. Kwa mujibu wa Mkude (2004) aina ya msamiati uliosukwa kimkakati na kuratibiwa kwa nia ya kuashiria dhana teule za taaluma fulani huitwa istilahi. Huu ni msamiati maalumu ambao umetokana na msamiati mpana wa lugha na kufanyiwa marekebisho ili kuhakikisha kwamba maana ya neno inaacha au inapanua maana yake ya kawaida na kubeba maana maalumu kwa ajili ya matumizi katika uwanja maalumu.
Ili kutekeleza majukumu yake kama chombo chenye mamlaka ya kukuza na kuimarisha Kiswahili kama lugha ya taifa na mojawapo ya lugha mbili rasmi za Tanzania, BAKITA linayo idara mahususi (Idara ya Kamusi na Istilahi) inayoshughulikia kusanifu istilahi kwa ajili ya kuziba pengo la kukosekana kwa istilahi katika nyanja mbalimbali. Kazi kubwa inayofanywa na idara hii ni kutafuta visawe vya Kiswahili vya istilahi za Kiingereza zilizopo tayari. Katika kufanya kazi hiyo BAKITA hupokea orodha za istilahi kama hizo baadhi huja tayari na mapendekezo ya visawe vya Kisahili vilivyopendekezwa na mletaji mwenyewe ili yapitiwe na kurekebishwa kama hapana budi au yathibitishwe ili baada ya kukubaliwa rasmi na BAKITA yasambaazwe na kuanza kutmika. Lakini kwa kiasi kikubwa orodha zinazoletwa huwa hazina mapendekezo yoyote ya visawe vya Kiswahili. Idara husika hufanya utafiti kutafuta visawe na kasha Kamati ya kuisanifu istilahi ya BAKITA hukaa na kutumia mbinu mbalimbali ili kuvipitia na kuvisanifu visawe hivyo. Ndipo visawe hivyo vinapowaslishwa katika kikao cha Baraza zima ili kutoa idhini na hatimaye kuvisambaza vianze kutumika. Mpaka sasa BAKITA limefaulu kusanifu na kusambaza istilahi zipatazo zaidi ya elfu 10 za nyanja maalumu na taaluma mbalimbali zaidi ya 30.
Lengo la makala hii ni kueleza misingi na mbinu ambazo BAKITA hutumia katika kuunda istilahi za Kiswahili. Vilevile makala itagusia matatizo yanayojitokeza wakati wa kuunda istilahi na pia baada ya kuunda istilahi.
2.0 Misingi na mbinu za uundaji wa istilahi
Shirika la Kimataifa la Viwango (ISO) ambalo miongoni mwa kazi zake ni kuratibu na kusimamia uendelezaji wa istilahi kimataifa, limeorodhesha kanuni zinazopaswa kufuatwa wakati wa kuunda istilahi katika lugha yoyote. Misingi hii imetokana hasa na mtazamo wa wanaisimu wa Vienna – yaani “Shule ya Istilahi ya Vienna (Austria)” iliyoanzishwa na Eugen Wuster. Kwa muhtasari kanuni hizo zinahusu uundaji wa istilahi lugha moja tu inapohusika na pale lugha mbili zinapohusika. Lugha moja inapohusika kanuni zifuatazo hazina budi zizingatiwe:
(1) Istilahi ziundwe baada ya kupata dhana iliyoelezwa kwa ukamilifu na wazi.
(2)
Istilahi ziwe fupi kadiri
iwezekanavyo lakini zenye kueleweka. Uundaji wa istilahi kwa vifupisho na
akronimia uepukwe hasa kama istilahi kamili si ndefu sana.
(3)
Sarufi ya lugha inayohusika lazima
itiliwe maanani. Kwa hiyo istilahi ziundwe kwa kufuata mofolojia ya kawaida ya
lugha.
(4)
Istilahi ziundwe kwa njia ambayo
itakuwa rahisi kuunda istilahi nyingine kwa mnyumbuliko.
(5)
Uundaji wa istilahi kwa kupanua
maana ya neno uepukwe hasa iwapo nyanja zinazotumia maneno hayo zinakaribiana,
ili kuepusha utata. Kwa hiyo mfumko wa sinonimia au homonimia (visawe) hauna
budi kuepukwa ili watumiaji wasikanganyikiwe.
Lugha mbili zinapohusika kanuni zifuatazo zizingatiwe:
(1) Uundaji wa istilahi kwa njia ya kukopa (kutohoa) maneno ya lugha nyingine uzingatie kuchukua maneno kama yalivyo katika lugha ya asili na kufanya marekebisho machache tu ili kulingana na sarufi na matamshi ya lugha pokezi.
(2) Uundaji wa istilahi kwa kutumia Kigiriki na Kilatini uendelezwe ili kuzingatia uwakilishi sahihi wa dhana hasa za sayansi na pia kupunguza kishawishi cha kupendelea kutumia baaadhi tu yalugha zinazotumika ulimwenguni hivi sasa.
Katika uzoevu wa kusanifu istilahi, BAKITA limekuwa likizingatia pia kanuni za nyongeza ili kupata ufanisi zaidi kwa kutilia maanani jamii ya watumiaji wa Kiswahili na utamaduni wake. Kubwa kati ya kanuni hizo za nyongeza ni:
(1) istilahi ziepuke utusani – yaani zisiundwe kwa maneno ambayo tayari yanaeleweka kwamba ni matusi kwa watumiaji. Kwa mfano katika kutafuta kisawe cha penis, neno mboo hushitua watumiaji wa Kiswahili wengi na badala yake neno dhakari huvumulika na kutumika zaidi. Kadhalika kisawe cha neno bone marrow neno uboho ingawa ni sanifu pia lakini huepukwa sana katika matumizi na badala yake neno uloto limekomaa sana katika matumizi. Vilevile katika kutafuta kisawe cha neno anus, neno mkundu hushitua watumiaji na neno ngoko likachukuliwa.
(2) Istilahi ziwe angavu vya kutosha – yaani istilahi ziweze kudokeza dhana liliyokusudiwa kwa kina na usahihi kadiri iwezekanavyo. Wakati wa kutafuta kisawe cha neno flip chart kwa Kiswahili kumekuwa na pendekezo la neno bango kitita. Katika kulichambua neno hilo imedhihirika ya kwamba ingawa neno bango kwa kiasi fulani linawakilisha ukubwa wa chart lakini dhana ya flip haijidhihirishi. Hivyo halina uangavu wa kutosha. Pendekezo linaloelekea kupendelewa ni chati pindu kwa kuwa neno hilo linawakilisha dhana ya chart na pia utumiksji wake wa kupinduliwa wakati chati hiyo inapotumiwa.
(3) Istilahi ziwe na ulinganifu wa mtiririko ulio katika dhana za kikoa kimoja. Katika hili ni muhimu kwa wasanifishaji kukumbuka kwamba istilahi hazikai pekepeke. Hazifiki mbali iwapo zitasimama pasipo kuhusisha maneno mengine yaliyo katika uga huo. Istilahi ni kama matundu ya wavu ambayo kila moja sharti ligusane na lenzake ili hatimaye mfumo mzima wa wavu uweze kutengenezwa. Kwa hiyo istilahi moja iwe chanzo cha kupata istilahi zingine kutokana na kuinyumbulisha na kuunda istilahi zinazohusiana katika uwanja ule. Kwa mfano: Sumaku (magnet), Usumaku (magnetism), Sumakisha (magnetise), Jisumakisha (auto magnetise), Usumakishaji (magnetization, nk.
(4) Istilahi zilizozoeleka au kukomaa kutokana na kutumika kwa muda mrefu zisibadilishwe. Kanuni hii ni muhimu sana katika ukubalifu wa istilahi zinazoundwa. Ni muhimu kabla ya kuunda istilahi mpya kuchunguza iwapo hakuna istilahi inayotumika tayari ambayo inawakilisha kw usahihi dhana inayokusudiwa. Uzoevu wa BAKITA umeonyesha kuwa ni vigumu kwa istilahi mpya kukubaliwa na kushamiri pale ambapo tayari kulikuwa na istiahi zilizokuwa zikitumika, hasa zile za muda mrefu. Kwa mfano neno Ovataimu (overtime) lililokuwa limezoeleka kwa muda mrefu limeendelea kutumika badala ya neno ajari. Vivyo hivyo neno Mdai (creditor) limeendelea kutumika badala ya neno Mwia. Maneno yote mawili ni ya siku nyingi lakini neno mdai limezagaa zaidi katika matumizi kuliko neno mwia.
3.0 Vyanzo vya istilahi
BAKITA linafuata utaratibu ufuatao ili kupata istilahi sanifu:
(a) Hazina ya Kiswahili
chenyewe
Hazina ya Kiswahili chenyewe huhusisha Kiswahili na lahaja nyingine za Kiswahili. Kwa kawaida kabla ya kutafuta kisawe cha Kiswahili cha istilahi iliyo katika lugha ngeni, wataalamu wa uwanja husika huhusishwa kikamilifu ili kueleza kwa ukamilifu dhana au maana ya istilahi hiyo kwa wajumbe wa Kamati ya Kusanifu Istilahi. Baada ya hapo wajumbe huanza kutafuta iwapo kuna kisawe katika Kiswahili Sanifu cha istilahi iliyotolewa. Kama kisawe hakipatikani katika Kiswahili Sanifu wajumbe hutafuta kama kuna neno katika lahaja za Kiswahili. Mifano michache jinsi mbinu hii ilivyotumika ni istilahi zifuatazo:
Chovyo (oedema) kutoka lahaja ya Kipemba
Mbolezi (elegiac poetry) kutoka lahaja ya Kimvita
Ng’ozi (leaf curl) kutoka lahaja ya Kimtang’ata
Kisabeho (breakfast) kutoka lahaja ya Kipemba (kutokana na Kitenzi kusabehe)
Kiangata (hob) kutoka lahaja za Kiamu na Kisiu
Hazina ya Kiswahili chenyewe pia huhusu mbinu mbalimbali zinazoweza kuunda maneno ya Kiswahili kwa njia ya kunyumbulisha mzizi waneno, kufinyaza maneno au kwa njia ya kuunganisha maneno:
Chakula cha jioni = Chajio
Chemchemi ya maji moto = Chemimoto
Mfupa wa paja = Fupaja
Hati ya kukataza kuiga = Hataza
Bara lililozama = Barazama
Matuta kama ngazi = Matungazi
Huduma hadi bandarini = Huhaba
Huduma hadi melini = Huhame
Utando mwembamba wa ogani = Utandogani
Teknolojia ya habari na mawasiliano = Teknohama nk.
Jambo la kuzingatia ni kwamba mbinu hii inapaswa itumiwe kwa uangalifu sana ili istilahi itakayotokana nayo iwasilishe dhana kwa usahihi na pia iwe na uangavu wa kutosha kwa watumiaji. Kama mojawapo kati ya sifa hizo ikipuuzwa istilahi haitakuwa sahihi ipasavyo na wala uangavu ukipuuzwa istilahi haitapata nguvu ya kusambaa na kushika mizizi baina ya watumiaji.
Mbinu hii hutumika hasa kwa lengo la kufupisha istilahi ndefu kwa kuondoa viunganifu au umilikaji.
Kipima pembe kwa ubapa = Kipimapembe ubapa
Doa la kutu = Doakutu
Nyundo ya rungu = Nyundorungu
Mwana + harakati = Mwanaharakati
Mwendo wa kasi = Mwendokasi
Nishati iliyotulia = Nishati tuli
Nishati yenye mwendo = Nishati mwendo
(b) Hazina ya
lugha za Kiafrika
Lugha za Kiafrika ni chanzo kingine ambacho husaidia kuunda visawe vya Kiswahili. Hazina hii hutumiwa pale hazina ya Kiswahili chenyewe inaposhindwa kukidhi haja ya kupata istilahi mwafaka inayoweza kuwakilisha dhana inayoshughulikiwa. Upendeleo hutolewa kwanza kwa lugha za Kibantu kwa sababu Kiswahili chenyewe ni mojawapo kati ya lugha za kundi hilo. Kwa hiyo maneno yanayotoka katika lugha za kundi hili hata yachukuliwapo katika Kiswahili yatakuwa na uangavu wa kutosha kwa watumiaji wa Kiswahili. Kwa sasa BAKITA limekuwa likitafuta maneno yaliyo katika lugha za Kibantu za Tanzania kuliko za nchi zingine. Jambo la kuzingatia kamam ilivyokwisha kudokezwa katika kanuni ya kukopa au kutohoa ni kwamba maneno yanayochukuliwa kutoka huko hurekebishwa ili yatii kanuni ya muundo wa Kiswahili hasa katika maumbo yake na pia jinsi yanavyopaswa yapatanishwe yatumikapo katika sentensi. Mifano michache kutoka hazina hii ni kama ifuatayo:
Neno la asili Istilahi Kisw) Umoja (Kisw) Wingi Upatanisho